Nazir Ayyad, mkuu wa Kituo cha Mafunzo ya Kiislamu cha Al-Azhar, alisema mkutano huo ulifanyika kwa kuzingatia jukumu la Al-Azhar kama chombo kinachosimamia uchapishaji na usambazaji wa nakala za Qur'ani Tukufu
Alisema Al-Azhar ina jukumu la kuzuia upotoshaji wowote katika nakala za Qur'ani Tukufu, tovuti ya Ad-Dustur iliripoti.
Amesema Al Azhar inadhibiti kikamilifu mchakato wa uchapishaji na usambazaji wa Qur'ani kwa kamati maalumu inayojumuisha wataalamu wa sayansi ya Qur'ani kutoka Kitivo cha Qur'ani cha Chuo Kikuu cha Al-Azhar.
Alisema katika kikao cha hivi majuzi kati ya maafisa wa Al-Azhar na wanachama wa chama cha wachapishaji, pande hizo mbili zilikubaliana kuharakisha mchakato wa kutoa ruhusa za uchapishaji wa Qur'ani.
Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na matatizo mengi katika uchapishaji wa Qur'an nchini Misri na baadhi ya nakala zilizochapishwa zenye makosa madogo madogo.
Pia, baadhi ya nakala zimechapishwa baada ya muda wa ruhusa ya uchapishaji kuisha huku nyingine zikiwa zimechapishwa kwa njia isiyo rasmi bila kupata kibali chochote. Misri ni nchi ya Afrika Kaskazini yenye wakazi wapatao milioni 100. Waislamu ni takriban asilimia 90 ya watu wote wa nchi hiyo.