Ukarabati wa Msikiti wa Al Hakim bi Amr Allah ulijumuisha urejeshaji taa kubwa ya dari, sakafu ya marumaru.
Msikiti huu wa Waislamu wa madhehebu ya Shia ambao unakadiriwa kujengwa miaka 1000 iliyopita na uko katikati ya mji wa Cairo ulifunguliwa tena Jumatatu kufuatia ukarabati mkubwa.
Kazi ya ukarabati wa Msikiti wa Al Hakim bi Amr Allah ilianza mwaka wa 2017 na ilijumuisha ukarabati wa kuta zake, kulingana na Brigedia Jenerali Hisham Samir, afisa wa wizara ya utalii na mambo ya kale ambaye alizungumza wakati wa kufungua tena eneo hilo la ibada.
Aidha amesema kumefanyika ukarabati katika milango ya mbao mimbari yake na dari katika msikiti huo ambao ni mojawapo ya maeneo mashuhuri zaidi ya enzi za Fatimiyya huko Cairo.
Ujenzi wa Msikiti wa Al Hakim bi Amr Allah ulianzishwa na khalifa Al Aziz mwaka wa 990 Miladia na ulikamilishwa na mwanawe, Al Hakim, khalifa wa sita wa zama za Fatimiyya, na hivyo msikiti huo ukapawa jina lake mwenyewe.
Tetemeko la ardhi la karne ya 14 Miladia liliharibu sehemu ya msikiti. Baadaya msikiti huo ulikarabatiwa kwa msaada wa viongozi kadhaa wa Kiislamu wa Misri. Aidha eneo la msikiti huo lilitumiwa na Napoleon wa Ufaransa kama makazi ya askari wake wakati wa kampeni ya kivita ya Ufaransa ya 1798 huko Misri na Syria.
Ukhalifa wa Fatimiyya ulikuwa ni miongoni mwa makundi mashuhuri ya Kiismaili na kundi pekee la Kishia lililowahi kutawala Misri. Wafattimi walitawala na Cairo kama mji mkuu wao na hadi leo turathi zao zingalipo mjini humo.
3482649