Taarifa kutoka Nigeria zinasema kuwa, mahakama imeakhirisha kusiikiliza kesi hiyo baada ya wafuasi wengi wa Sheikh Zakzaky kujitiokeza na kuandamana wakipinga kesi dhidi ya kiongozi wao huyo na badala yake wanataka aachiliwe huru.
Jana vikosi vya usalama nchini Nigeria vilikandamiza maandamano ya wafuasi wa Sheikh Zakzaky kwa kufyatua risasi ambapo raia mmoja aliuawa shahidi na mwengine kadhaa kujeruhiwa.
Kesi ya Sheikh Ibrahim Zakzaky ambayo ilianza kusikilizwa tangu Novemba mwaka jana bila ya yeye kuhudhuria mahakamani, iliendelea tena Jumatatu ya juzi kwa mahakama kusikiliza upande wa mashahidi. Kesi hiyo ilitarajiwa kuendelea tena jana Jumanne, lakini sasa imeakhirishwa.
Wafuasi wa Sheikh Zakzaky wamekuwa wakivitaka vyombo vya usalama vimuachilie huru kiongozi huyo pamoja na mkewe kwani hawana hatia yoyote kwa mujibu wa amri ya iliyowahji kutolewa huko nyuma na mahakama.
Wakati huo huo, mke wa Sheikh Ibrahim Zakzaky, Malama Zeenat ambaye alikuwa akishikiliwa kizuizini pamoja na mumewe hivi karibuni alihamishiwa hospitali kwa amri ya mahakama baada ya kuambukizwa virusi vya Corona.
Sheikh Ibrahim Zakzaky na mke wake walikamatwa na vyombo vya dola vya Nigeria tarehe 13 Disemba mwaka 2015 katika shambulizi lililofanywa na askari wa nchi hiyo dhidi ya kituo cha kidini cha Baqiyyatullah katika mji wa Zaria.
Karibu wafuasi 1,000 wa harakati ya Kiislamu ya Nigeria waliuawa kwa umati na vikosi vya usalama katika shambulizi hilo.