Harakati ya Hizbullah imetoa taarifa ikieleza kuwa kundi la mashahidi Hassan Zebib na Yassir Tahir ndilo lililotekeleza oparesheni hiyo Jumapili Alasiri. Televisheni ya al Aalam pia imeripoti kuwa jeshi la Israel limewaagiza wakazi wa maeneo ya mpakani na Lebanon kusalia majumbani. Televisheni ya al Jazeera pia imevinukuu vyombo vya habari vya jeshi la Israel na kutangaza kuwa: Jeshi hilo limewataka wakazi wa maeneo ya kandokando na mipaka ya Lebanon yaliyoko katika umbali wa kilomita nne.
Ripoti zilizotufikia zinasema kuwa, Benjamin Netanyahu Waziri Mkuu wa utawala wa Israel ameelekea katika Wizara ya Vita ya utawala huo kwa ajili ya kikao cha dharura pamoja na wakuu wa majeshi na wa idara za intelijinsia za utawala ili kufuatilia hali ya mambo inayoendelea sasa katika mipaka ya Lebanon.
Vyombo vya habari vya Lebanon aidha vimetangaza kuwa jeshi la Israel limetumia risasi zenye mada za fosiforasi kushambulia maeneo ya kandokando mwa Maroun al Ras kusini mwa Lebanon.
Siku moja kabla ya oparesheni hiyo, Katibu Mkuu wa Hizbullah Sayyid Hassan Nasrallah, akizungumza kwa munasaba wa kuanza Mwezi wa Muharram, alisema kwa kutumia mbinu maalumu na kulingana na irada yake na kwa namna utakavyotaka, Hizbullah itachagua wakati, mahali na mazingira mwafaka kwa ajili ya kutoa jibu kwa uvamizi uliofanywa na Israel.
Sayyid Hassan Nasrallah alibainisha kuwa, Hizbullah inacho kiwango cha kutosha cha makombora yanayolenga shabaha kwa umakini na kusisitiza kwamba, muqawama uko tayari kwa makabiliano yoyote yale madogo au makubwa na adui Israel.
Katika muda wa wiki moja iliyopita, ndege zisizo na rubani za utawala wa Kizayuni zimekiuka mara tatu mipaka ya anga ya Lebanon.
Na hii ni pamoja na kwamba, baada ya kumalizika vita vya siku 33 vya mwaka 2006 vilivyoanzishwa na Israel dhidi ya Lebanon, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio nambari 1701, ambalo liliutahadharisha utawala huo wa Kizayuni na uchukuaji hatua zozote za kiuadui dhidi ya Lebanon; lakini utawala huo limelipuuza azimio hilo na kuendelea kukiuka kila mara mipaka ya anga, ardhini na baharini ya nchi hiyo.