IQNA

Walowezi wa Kizayuni walivunjia heshima kaburi la Nabii Yusuf (AS)

22:48 - April 08, 2016
Habari ID: 3470234
Walowezi wa Kizayuni wasiopungua 1,000 waliokuwa wakisindikizwa na askari wa utawala haramu wa Israel wamevamia na kulivunjia heshima kaburi la Nabii Yusuf (AS), ziara linaloheshimiwa na Wayahudi, Wakristo na Waislamu.

Duru za usalama za Palestina pamoja na wakaazi wa viunga vya mji wa Nablus, katika Ufukwe wa Magharibi wa Mto Jordan ambako ndipo lilipo kaburi hilo wamesema, walowezi hao wa Kizayuni waliwasili mahala hapo mapema Alkhamisi wakiwa ndani ya mabasi kadhaa na kuvamia ziara hilo huku wakipewa ulinzi na askari wa utawala haramu wa Israel.

Vikosi vya utawala wa Kizayuni viliweka magari kadhaa ya kijeshi katika barabara inayoelekea kwenye haram ya Nabii Yusuf ili kuzuia kutokea mapigano baina ya Wapalestina na walowezi hao wa Kizayuni.

Muda mfupi baadaye yalizuka makabiliano baina ya askari wa Kizayuni na vijana wa Kipalestina kandokando ya eneo lilipo kaburi la Nabii Yusuf, ambapo askari hao walitumia gesi ya kutoa machozi kuwatawanya vijana wa Kipalestina.

Tukio hilo limejiri siku moja tu baada ya askari wa jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel na maafisa usalama wa utawala huo ghasibu kuvamia eneo moja la ardhi huko Ras al-Amud karibu na Baitul Muqaddas mashariki na kung'oa miche 47 ya mizaituni iliyokuwa imepandwa na Wapalestina kwa heshima ya kuwaenzi Wapaletsina 47 waliouliwa shahidi na askari wa Kizayuni katika mji huo mtukufu tangu ilipoanza Intifadha mwezi Oktoba mwaka jana.

Wapalestina wasiopungua 210 wakiwemo wanawake na watoto wameshauliwa shahidi hadi sasa na askari wa utawala haramu wa Israel tangu ilipoanza Intifadha ya Quds.
3459469
captcha