Kongamano hilo litakalofanyika mjini Tehran Jumapili Novemba Mosi litawaleta pamoja washiriki Wairani na kutoka nchi za kigeni ambao wameandika makala zipatazo 640.
Kongamano hilo la kimataifa limekuwa likiandaliwa kwa muda wa mwaka moja chini ya uenyekiti wa Waziri wa Utamaduni na Muongozo wa Kiislamu Iran Ali Jannati. Taasisi ya Utafiti ya Imam Khomeini MA imekuwa ikifanya kazi za kitaalamu za kongamano hilo.
Naibu Waziri wa Utamaduni na Muongozo wa Kiislamu anayesimamia masuala ya Qur’ani Hujjatul Islam Muhammad Ridha amesema kongamano hilo litajadili maudhui kama vile, ‘Umuhimu wa Qur’ani kwa Mtazamo wa Imam Khomeini MA,’ ‘Misingi ya Tafsiri ya Qur’ani Kwa Mtazamo wa Imam Khomeini MA’, ‘Dhihirisho la Mafundisho ya Qur’ani Katika Mafundisho ya Kisiasa na Sirah ya Kijamii ya Imam Khomeini MA’ na ‘Maadili ya Qur’ani Katika Vitendo na Maneno ya Imam Khomeini MA.’