IQNA

Waislamu Marekani

Benki za Marekani zatakiwa kukomesha ubaguzi dhidi ya Waislamu

19:11 - December 03, 2022
Habari ID: 3476191
TEHRAN (IQNA) - Wabunge kadhaa nchini Marekani wamezitaka benki za nchi hiyo kuacha mbinu za kibaguzi dhidi ya Waislamu.

Mwakilishi Ilhan Omar  na Seneta Elizabeth Warren  ambao wote ni wa chama  cha Democrat walisambaza barua siku ya Ijumaa wakimtaka mkuu wa wadhibiti wa benki nchini Marekani kutathmini upya sera zinazowabagua kikamilifu Waislamu Wamarekani na watu wengine wasio wazungu.

"Watu wasiohesabika wa Marekani, biashara, na mashirika ya kutoa misaada yamekuwa wahasiriwa wa sera na mazoea ya kibaguzi ambayo yanaonekana kuwazuia kupata huduma za kifedha kwa sababu ya dini zao au asili ya kitaifa," imesema barua hiyo iliyotiwa saini na zaidi ya wabunge 12. "Waislamu wengi na Waarabu, Waamerika wengi wa Mashariki ya Kati na Kusini mwa Asia, kwa sababu tu ya uhusiano wao - wa kweli au unaofikiriwa - wamekatiliwa mbali kutoka kwa huduma za kifedha," wabunge waliandika.

Kwa Waislamu wa Marekani na watu binafsi kutoka nchi zilizoathiriwa na vikwazo vya Marekani, kuendesha akaunti ya benki au kutuma pesa nje ya nchi kumesababisha msururu wa changamoto ambazo wengi wanasema ni ubaguzi wa rangi. Watu wanasema wamekuwa wakilengwa na taasisi za fedha kulingana na asili yao ya kidini na kikabila au kikaumu, ikiwa ni pamoja na kufungiwa akaunti zao za benki bila ya onyo, malipo yao kwa wapendwa wao nje ya nchi na akaunti zao kuchunguzwa isivyo haki.

Mnamo 2019, mwanamke Mwislamu aliwasilisha malalamiko dhidi ya Citibank huko New York baada ya benki hiyo kudaiwa kumzuia kufungua akaunti, ikisema walihitaji kwanza kumchunguza mumewe, ambaye ana jina la mwisho la Kiarabu. Mnamo mwaka wa 2017, mwanamume Mwislamu, mkewe, na bintiye mwenye umri wa miaka 15 walizuiliwa na polisi wakati karani wa kupokea fedha benki alipopiga alipopigia polisi simu alipokuwa akijaribu kuweka hundi.

Wamarekani Waislamu ambao wanaendesha mashirika yasiyo ya faida pia wamesema kuwa mashirika yao ya kutoa misaada yamefungwa bila sababu. Ripoti ya 2014 ya The Los Angeles Times ilipata takriban kufungwa kwa akaunti kumi na mbili zinazohusisha Waislamu na wahamiaji kutoka Mashariki ya Kati na mashirika yao yasiyo ya faida.

Barua hiyo, ambayo inawauliza wakuu wa benki ni hatua gani za kurekebisha zitachukuliwa, inataka jibu ndani ya siku 30 katika kushughulikia maswala ya ubaguzi na utekelezwaji wa vikwazo, kati ya maswala mengine.

3481505

captcha