IQNA

Kiongozi Muadhamu katika Mkutano na Waziri Mkuu wa Pakistan

Kumalizika ipasavyo vita Yemen kutakuwa na taathira chanya katika eneo

21:29 - October 13, 2019
Habari ID: 3472169
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kwa muda sasa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imewasilisha mpango wa nukta nne wa kumaliza vita nchini Yemen na kuongeza kuwa: "Iwapo vita hivyo vitamalizika ipasavyo, basi jambo hilo linaweza kuwa na taathira chanya katika eneo.

Ayatullah Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo Jumapili alasiri mjini Tehran wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Pakistan Imran Khan. Katika kikao hicho, Kiongozi Muadhamu amesema uhusiano wa Iran na Pakistan ni wa kina sana na unajumuisha pia wananchi na kwa msingi huo amebaini ulazima wa kutumia msingi huo kuimarisha ushirikiano wa nchi mbili.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria mfano wa kina na wa karibu na wa wananchi wa mataifa mawili ya Pakistan na Iran na kusema: "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaitazama Pakistan kama ndugu na jirani."
Ayatullah Khamenei ameongeza kuwa: "Kutokana na kuwepo fursa hii ya kipekee, uhusiano wa nchi mbili unapaswa kuwa bora zaidi na usalama wa mipakani uimarishwe na mpango uliochelewa wa bomba la gesi ukamilike."
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameipongeza serikali ya Pakistan kutokana kujali kwake kuhusu kuwepo amani na usalama na kuongeza kuwa eneo la Asia Magharibi ni nyeti na hatari mno. Ayatullah Khamenei amesisitiza kuhusu wote kuwa waangalifu ili kuzuia kuibuka maafa huku akibainisha masikitiko yake kutokana na nafasi haribifu ya baadhi ya nchi za eneo katika kuunga mkono makundi ya kigaidi Iraq na Syria na kuibua vita na umwagaji ndamu nchini Yemen.
Ameongeza kuwa: "Sisi hatuna sababu ya kuwa na uhasama na nchi hizo lakini ziko chini ya irada ya Marekani na zinatekeleza sera zao dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa mujibu wa matakwa ya Marekani.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu haijawahi kuanzisha vita vyovyote na kuongeza kuwa: "Lakini iwapo yeyote ataanzisha vita dhidi ya Iran, bila shaka atajuta."
Imran Khan Waziri Mkuu wa Pakistan akizungumza katika kikao hicho amesema Iran na Pakistan ni nchi ndugu na kuongeza kuwa: "Ushirikiano wa Tehran na Islamabad unapaswa kuimarika." Amesema nchi yake inalipa umuhimu wa kipekee suala la uhusiano na Iran kwa sababu Iran ni mshirika mkubwa wa Pakistan kibiashara.

Wakati huo huo, Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, Tehran na Islamabad zinaamini kuwa, masuala ya kieneo yanapaswa kutatuliwa kwa njia ya mazungumzo baina ya nchi mbalimbali.

Rais Hassan Rouhani ameyasema hayo  mjini Tehran mbele ya waandishi wa habari akiwa pamoja na Waziri Mkuu wa Pakistan Imran Khan na kuongeza kuwa: Katika mazungumzo yao pande hizo mbili zimetilia mkazo umuhimu wa amani ya eneo nyeti la Ghuba ya Uajemi na kwamba, ufunguo wa utatuzi wa masuala ya eneo hilo ni kukomeshwa vita vya Yemen na kusitisha mapigano mara moja. 

 Rais Rouhani pia ameashiria vikwazo vya Marekani dhidi ya wananchi wa Iran na kusema: Katika mazungumzo haya pande mbili zimevitaja vikwazo vya Marekani dhidi ya taifa la Iran kuwa ni ugaidi wa kiuchumi na kutangaza kuwa, Marekani inapaswa kurejea kwenye makubaliano ya nyuklia ya JCPOA na kufuta vikwazo hivyo ili kuweza kutatua kadhia hiyo. 

3849667/

captcha